Maktaba yote ya Kiislamu

89 - The Dawn - Al-Fajr

:1

Naapa kwa alfajiri,

:2

Na kwa masiku kumi,

:3

Na kwa viwili viwili na kimoja kimoja,

:4

Na kwa usiku unapo pita,

:5

Je! Hapana katika haya kiapo kwa mwenye akili?

:6

Kwani hukuona jinsi Mola wako Mlezi alivyo wafanya kina A'di?

:7

Wa Iram, wenye majumba marefu?

:8

Ambao haukuumbwa mfano wake katika nchi?

:9

Na Thamudi walio chonga majabali huko bondeni?

:10

Na Firauni mwenye vigingi?

:11

Ambao walifanya jeuri katika nchi?

:12

Wakakithirisha humo ufisadi?

:13

Basi Mola wako Mlezi aliwapiga mjeledi wa adhabu.

:14

Hakika Mola wako Mlezi yupo kwenye mavizio anawavizia.

:15

Ama mtu anapo jaribiwa na Mola wake Mlezi, akamkirimu na akamneemesha, husema: Mola wangu Mlezi amenikirimu!

:16

Na ama anapo mjaribu akampunguzia riziki yake, husema: Mola wangu Mlezi amenitia unyonge!

:17

Sivyo hivyo! Bali nyinyi hamuwakirimu mayatima,

:18

Wala hamhimizani kulisha masikini;

:19

Na mnakula urithi kwa ulaji wa pupa,

:20

Na mnapenda mali pendo la kupita kiasi.

:21

Sivyo hivyo! Itakapo vunjwa ardhi vipande vipande,

:22

Na akaja Mola wako Mlezi na Malaika safu safu,

:23

Na ikaletwa Jahannamu siku hiyo, siku hiyo mtu atakumbuka! Lakini kukumbuka huko kutamfaa nini?

:24

Atasema: Laiti ningeli jitangulizia kwa uhai wangu!

:25

Basi siku hiyo hataadhibu yeyote namna ya kuadhibu kwake.

:26

Wala hatafunga yeyote kama kufunga kwake.

:27

Ewe nafsi iliyo tua!

:28

Rejea kwa Mola wako Mlezi umeridhika, na umemridhisha.

:29

Basi ingia miongoni mwa waja wangu,

:30

Na ingia katika Pepo yangu.