Maktaba yote ya Kiislamu

83 - The Defrauding - Al-Muţaffifīn

:1

Ole wao hao wapunjao!

:2

Ambao wanapo jipimia kwa watu hudai watimiziwe.

:3

Na wao wanapo wapimia watu kwa kipimo au mizani hupunguza.

:4

Kwani hawadhani hao kwamba watafufuliwa

:5

Katika Siku iliyo kuu,

:6

Siku watapo msimamia watu Mola Mlezi wa walimwengu wote?

:7

Hasha! Hakika maandiko ya wakosefu bila ya shaka yamo katika Sijjin.

:8

Unajua nini Sijjin?

:9

Kitabu kilicho andikwa.

:10

Ole wao siku hiyo kwa wanao kadhibisha!

:11

Ambao wanaikadhibisha Siku ya Malipo.

:12

Wala haikadhibishi ila kila mwenye kuruka mipaka, mwenye dhambi.

:13

Anapo somewa Aya zetu husema: Ni visa vya watu wa kale!

:14

Hasha! Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao hao walio kuwa wakiyachuma.

:15

Hasha! Hakika hao siku hiyo bila ya shaka watazuiliwa na neema za Mola wao Mlezi.

:16

Kisha wataingia Motoni!

:17

Kisha waambiwe: Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyakadhabisha.

:18

Hasha! Hakika maandiko ya watu wema bila ya shaka yamo katika I'liyyin.

:19

Na nini kitakacho kujuvya nini I'liyyin?

:20

Kitabu kilicho andikwa.

:21

Wanakishuhudia walio karibishwa.

:22

Hakika watu wema bila ya shaka watakuwa katika neema.

:23

Wakae juu ya viti vya enzi wakiangalia.

:24

Utatambua katika nyuso zao mng'aro wa neema,

:25

Watanyweshwa kinywaji safi kiliyo tiwa muhuri,

:26

Muhuri wake ni miski. Na katika hayo washindanie wenye kushindana.

:27

Na mchanganyiko wake ni Tasniim,

:28

Chemchem watakayo inywa walio kurubishwa.

:29

Kwa hakika wale walio kuwa wakosefu walikuwa wakiwacheka walio amini.

:30

Na wanapo pita karibu yao wakikonyezana.

:31

Na wanapo rudi kwa watu wao hurudi nao wamefurahi.

:32

Na wanapo waona husema: Hakika hawa ndio khasa walio potea.

:33

Na wao hawakutumwa wawe walinzi juu yao.

:34

Basi leo walio amini ndio watawacheka makafiri,

:35

Nao wako juu ya viti vya enzi wakiangalia.

:36

Je! makafiri wamelipwa malipo ya yale waliyo kuwa wakiyatenda?