Maktaba yote ya Kiislamu

79 - Those who drag forth - An-Nāzi`āt

:1

Naapa kwa wanao komoa kwa nguvu,

:2

Na kwa wanao toa kwa upole,

:3

Na wanao ogelea,

:4

Wakishindana mbio,

:5

Wakidabiri mambo.

:6

Siku kitapo tetemeka cha kutetemeka,

:7

Kifuate cha kufuatia.

:8

Siku hiyo nyoyo zitapiga piga,

:9

Macho yatainama chini.

:10

Sasa wanasema: Ati kweli tutarudishwa kwenye hali ya kwanza?

:11

Hata tukiwa mifupa iliyo bunguliwa?

:12

Wanasema: Basi marejeo hayo ni yenye khasara!

:13

Kwa hakika hayo ni ukelele mmoja tu,

:14

Mara watakuwa kwenye uwanda wa mkutano!

:15

Je! Imekufikia hadithi ya Musa?

:16

Mola wake Mlezi alipo mwita katika bonde takatifu la T'uwaa, akamwambia:

:17

Nenda kwa Firauni. Hakika yeye amezidi jeuri.

:18

Umwambie: Je! Unapenda kujitakasa?

:19

Nami nitakuongoa ufike kwa Mola wako Mlezi, upate kumcha.

:20

Basi alimwonyesha Ishara kubwa.

:21

Lakini aliikadhibisha na akaasi.

:22

Kisha alirudi nyuma, akaingia kufanya juhudi.

:23

Akakusanya watu akanadi.

:24

Akasema: Mimi ndiye Mola wenu Mlezi mkuu kabisa.

:25

Basi hapo Mwenyezi Mungu akamshika kumuadhibu kwa la mwisho na la mwanzo.

:26

Kwa hakika katika haya yapo mazingatio kwa wanao ogopa.

:27

Je! Ni vigumu zaidi kukuumbeni nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliye ijenga!

:28

Akainua kimo chake, na akaitengeneza vizuri.

:29

Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana wake.

:30

Na juu ya hivyo ameitandaza ardhi.

:31

Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake,

:32

Na milima akaisimamisha,

:33

Kwa nafuu yenu na mifugo yenu.

:34

Basi itakapo fika hiyo balaa kubwa,

:35

Siku ambayo mtu atakumbuka aliyo yafanya,

:36

Na Jahannamu itadhihirishwa kwa mwenye kuona,

:37

Basi ama yule aliye zidi ujeuri,

:38

Na akakhiari maisha ya dunia,

:39

Kwa hakika Jahannamu ndiyo makaazi yake!

:40

Na ama yule anaye ogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi, na akajizuilia nafsi yake na matamanio,

:41

Basi huyo, Pepo itakuwa ndiyo makaazi yake!

:42

Wanakuuliza Saa (ya Kiyama) itakuwa lini?

:43

Una nini wewe hata uitaje?

:44

Kwa Mola wako Mlezi ndio mwisho wake.

:45

Kwa hakika wewe ni mwonyaji tu kwa mwenye kuikhofu.

:46

Ni kama kwamba wao siku watapo iona (hiyo Saa) hawakukaa ila jioni moja tu, au mchana wake.