Maktaba yote ya Kiislamu

69 - The Reality - Al-Ĥāqqah

:1

Tukio la haki.

:2

Nini hilo Tukio la haki?

:3

Na nini kitakujuulisha nini hilo Tukio la haki?

:4

Thamudi na A'di waliukadhibisha Msiba unao situsha.

:5

Basi Thamudi waliangamizwa kwa balaa kubwa mno.

:6

Na ama A'di waliangamizwa kwa upepo mkali usio zuilika.

:7

Alio wapelekea masiku saba, na siku nane, mfululizo bila ya kusita. Utaona watu wamepinduka kama kwamba ni magongo ya mitende yalio wazi ndani.

:8

Basi je! Unamwona mmoja wao aliye baki?

:9

Na Firauni na walio mtangulia, na miji iliyo pinduliwa chini juu, walileta khatia.

:10

Wakamuasi Mtume wa Mola wao Mlezi, ndipo Yeye Mola akawakamata kwa mkamato ulio zidi nguvu.

:11

Maji yalipo furika Sisi tulikupandisheni katika safina,

:12

Ili tuyafanye hayo kuwa ni waadhi kwenu na kila sikio linalo sikia liyahifadhi.

:13

Na litapo pulizwa barugumu mpulizo mmoja tu,

:14

Na ardhi na milima ikaondolewa, na ikavunjwa kwa mvunjo mmoja,

:15

Siku hiyo ndio Tukio litatukia.

:16

Na mbingu zitapasuka, kwani siku hiyo zitakuwa dhaifu kabisa.

:17

Na Malaika watakuwa pembezoni mwa mbingu; na wanane juu ya hawa watakuwa wamebeba Kiti cha Enzi cha Mola wako Mlezi.

:18

Siku hiyo mtahudhurishwa - haitafichika siri yoyote yenu.

:19

Basi ama atakaye pewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia, atasema: Haya someni kitabu changu!

:20

Hakika nalijua ya kuwa nitapokea hisabu yangu.

:21

Basi yeye atakuwa katika maisha ya kupendeza,

:22

Katika Bustani ya juu,

:23

Matunda yake yakaribu.

:24

Waambiwe: Kuleni na mnywe kwa furaha kwa sababu ya mlivyo tanguliza katika siku zilizo pita.

:25

Na ama atakaye pewa kitabu chake katika mkono wake wa kushoto, basi yeye atasema: Laiti nisingeli pewa kitabu changu!

:26

Wala nisingeli jua nini hisabu yangu.

:27

Laiti mauti ndiyo yangeli kuwa ya kunimaliza kabisa.

:28

Mali yangu hayakunifaa kitu.

:29

Madaraka yangu yamenipotea.

:30

(Pasemwe): Mshikeni! Mtieni pingu!

:31

Kisha mtupeni Motoni!

:32

Tena mtatizeni katika mnyororo wenye urefu wa dhiraa sabiini!

:33

Kwani huyo hakika alikuwa hamuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu,

:34

Wala hahimizi kulisha masikini.

:35

Basi leo hapa hana jamaa wa kumwonea uchungu,

:36

Wala hana chakula ila usaha wa watu wa Motoni.

:37

Chakula hicho hawakili ila wakosefu.

:38

Basi naapa kwa mnavyo viona,

:39

Na msivyo viona,

:40

Kwa hakika hii ni kauli iliyo letwa na Mjumbe mwenye hishima.

:41

Wala si kauli ya mtunga mashairi. Ni machache sana mnayo yaamini.

:42

Wala si kauli ya kuhani. Ni machache mnayo yakumbuka.

:43

Ni uteremsho utokao kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:44

Na lau kama angeli tuzulia baadhi ya maneno tu,

:45

Bila ya shaka tungeli mshika kwa mkono wa kulia,

:46

Kisha kwa hakika tungeli mkata mshipa mkubwa wa moyo!

:47

Na hapana yeyote katika nyinyi ambaye angeli weza kutuzuia.

:48

Kwa hakika hii ni mawaidha kwa wachamngu.

:49

Na hakika Sisi bila ya shaka tunajua kwamba miongoni mwenu wapo wanao kadhibisha.

:50

Na hakika bila ya shaka itakuwa ni majuto kwa wanao kataa.

:51

Na hakika hii bila ya shaka ni haki ya yakini.

:52

Basi litakase jina la Mola wako Mlezi Mtukufu.