Maktaba yote ya Kiislamu

68 - The Pen - Al-Qalam

:1

Nuun. Naapa kwa kalamu na yale wayaandikayo,

:2

Kwa neema ya Mola wako Mlezi wewe si mwendawazimu.

:3

Na kwa hakika wewe una malipo yasiyo katika.

:4

Na hakika wewe una tabia tukufu.

:5

Karibu utaona, na wao wataona,

:6

Ni nani kati yenu aliye pandwa na wazimu.

:7

Hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye ajuaye zaidi nani aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka.

:8

Basi usiwat'ii wanao kadhibisha.

:9

Wanatamani lau unge lainisha ili nao wakulainishie.

:10

Wala usimt'ii kila mwingi wa kuapa wa kudharauliwa,

:11

Mtapitapi, apitaye akifitini,

:12

Mwenye kuzuia kheri, dhaalimu, mwingi wa madhambi,

:13

Mkavu, na juu ya hayo, mshari, amejipachika tu.

:14

Ati kwa kuwa ana mali na watoto!

:15

Anapo somewa Aya zetu, husema: Hizi ni simulizi za uwongo za watu wa zamani!

:16

Tutamtia kovu juu ya pua yake.

:17

Hakika tumewajaribu hawa kama tulivyo wajaribu wale wenye shamba, walipo apa kwamba watayavuna mazao yake itakapo kuwa asubuhi.

:18

Wala hawakusema: Mungu akipenda!

:19

Basi lilitokea tukio juu yake kutoka kwa Mola wako Mlezi, nao wamelala!

:20

Likawa kama usiku wa giza.

:21

Asubuhi wakaitana.

:22

Ya kwamba nendeni kondeni mwenu ikiwa mnataka kuvuna.

:23

Basi walikwenda na huku wakinong'onezana,

:24

Ya kuwa leo hata masikini mmoja asikuingilieni.

:25

Na walikwenda asubuhi, nao wameshikilia azimio hilo.

:26

Basi walipo liona, wakasema: Hakika tumepotea!

:27

Bali tumenyimwa!

:28

Mbora wao akasema: Sikukwambieni, kwa nini hamumtakasi Mwenyezi Mungu?

:29

Wakasema: Ametakasika Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tulikuwa wenye kudhulumu.

:30

Basi wakakabiliana kulaumiana wao kwa wao.

:31

Wakasema: Ole wetu! Tulikuwa tumeikiuka mipaka!

:32

Asaa Mola wetu Mlezi akatubadilishia lilio bora kuliko hili. Hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.

:33

Namna hivi yanakuwa mateso, na bila ya shaka mateso ya Akhera ni makubwa zaidi, laiti wangeli jua!

:34

Hakika wachamngu watakuwa na Bustani za neema kwa Mola wao Mlezi.

:35

Kwani tutawafanya Waislamu kama wakosefu?

:36

Mna nini? Mnahukumu vipi?

:37

Au mnacho kitabu ambacho ndani yake mnasoma?

:38

Kuwa mtapata humo mnayo yapenda?

:39

Au mnazo ahadi za viapo juu yetu za kufika Siku ya Kiyama ya kuwa hakika mtapata kila mnayo jihukumia?

:40

Waulize: Ni nani miongoni mwao dhamini wa haya?

:41

Au wanao washirika? Basi wawalete washirika wao wakiwa wanasema kweli.

:42

Siku utakapo wekwa wazi mundi, na wataitwa kusujudu, lakini hawataweza,

:43

Macho yao yatainama chini, fedheha itawafunika. Na hakika walikuwa wakiitwa wasujudu walipo kuwa wazima -

:44

Basi niache na wanao kadhibisha maneno haya! Tutawavutia kidogo kidogo kwa mahali wasipo pajua.

:45

Na ninawapururia muhula; hakika hila zangu ni imara.

:46

Au unawaomba ujira, na wao wanaemewa na gharama hiyo?

:47

Au iko kwao siri, basi wao wanaiandika?

:48

Basi ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi, wala usiwe kama mmezwa na samaki, alipo nadi naye kazongwa.

:49

Kama isingeli mfikia neema kutoka kwa Mola wake Mlezi, bila ya shaka angeli tupwa ufukweni naye ni mwenye kulaumiwa.

:50

Lakini Mola wake Mlezi alimteua na akamfanya miongoni mwa watu wema.

:51

Na walio kufuru hukaribia kukutelezesha kwa macho yao, wanapo sikia mawaidha, na wanasema: Hakika yeye ni mwendawazimu.

:52

Na hayakuwa haya, ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote.