Maktaba yote ya Kiislamu

70 - The Ascending Stairways - Al-Ma`ārij

:1

Muulizaji aliuliza juu ya adhabu itakayo tokea,

:2

Kwa makafiri - ambayo hapana awezaye kuizuia -

:3

Kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye mbingu za daraja.

:4

Malaika na Roho hupanda kwendea kwake katika siku ambayo kadiri yake ni miaka khamsini elfu!

:5

Basi subiri kwa subira njema.

:6

Hakika wao wanaiona iko mbali,

:7

Na Sisi tunaiona iko karibu.

:8

Siku ambayo mbingu zitakapo kuwa kama maadeni iliyo yayushwa.

:9

Na milima itakuwa kama sufi.

:10

Wala jamaa hatamuuliza jamaa yake.

:11

Ijapo kuwa wataonyeshwa waonane. Atatamani mkosefu lau ajikomboe na adhabu ya siku hiyo kwa kuwatoa fidia wanawe,

:12

Na mkewe, na nduguye,

:13

Na jamaa zake walio kuwa wakimkimu,

:14

Na wote waliomo duniani, kisha aokoke yeye.

:15

La, hasha! Kwa hakika huo ni Moto mkali kabisa,

:16

Unao babua ngozi ya kichwa!

:17

Utamwita kila aliye geuza mgongo na akageuka.

:18

Na akakusanya mali, kisha akayahifadhi.

:19

Hakika mtu ameumbwa na papara.

:20

Inapo mgusa shari hupapatika.

:21

Na inapo mgusa kheri huizuilia.

:22

Isipo kuwa wanao sali,

:23

Ambao wanadumisha Sala zao,

:24

Na ambao katika mali yao iko haki maalumu

:25

Kwa mwenye kuomba na anaye jizuilia kuomba;

:26

Na ambao wanaisadiki Siku ya Malipo,

:27

Na ambao wanaiogopa adhabu itokayo kwa Mola wao Mlezi.

:28

Hakika adhabu ya Mola wao Mlezi si ya kuaminika nayo.

:29

Na ambao wanahifadhi tupu zao.

:30

Isipo kuwa kwa wake zao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, basi hao hawalaumiwi -

:31

Lakini wanao taka kinyume ya haya, basi hao ndio wanao ruka mipaka.

:32

Na ambao wanazichunga amana zao na ahadi zao,

:33

Na ambao wanasimama imara katika ushahidi wao,

:34

Na ambao wanazihifadhi Sala zao.

:35

Hao ndio watakao hishimiwa Peponi.

:36

Wana nini wale walio kufuru wanakutumbulia macho tu?

:37

Makundi kwa makundi upande wa kulia na upande wa kushoto!

:38

Kwani kila mmoja wao anatumai kuingizwa katika Pepo ya neema?

:39

La, hasha! Hakika Sisi tumewaumba kutokana na wanacho kijua.

:40

Basi naapa kwa Mola Mlezi wa mashariki zote na magharibi zote kwamba Sisi tunaweza

:41

Kuwabadili kwa walio bora kuliko wao; na Sisi hatushindwi.

:42

Basi waache wapige porojo na wacheze, mpaka wakutane na siku yao wanayo ahidiwa,

:43

Siku watakapotoka makaburini kwa upesi kama kwamba wanakimbilia mfundo,

:44

Macho yao yatainama, fedheha itawafunika. Hiyo ndiyo Siku waliyo kuwa wakiahidiwa.