Maktaba yote ya Kiislamu

51 - The Winnowing Winds - Adh-Dhāriyāt

:1

Naapa kwa pepo zinazo tawanya,

:2

Na zinazo beba mizigo,

:3

Na zinazo kwenda kwa wepesi.

:4

Na zinazo gawanya kwa amri,

:5

Hakika mnayo ahidiwa bila ya shaka ni kweli,

:6

Na kwa hakika malipo bila ya shaka yatatokea.

:7

Naapa kwa mbingu zenye njia,

:8

Hakika nyinyi bila ya shaka mmo katika kauli inayo khitalifiana.

:9

Anageuzwa kutokana na haki mwenye kugeuzwa.

:10

Wazushi wameangamizwa.

:11

Ambao wameghafilika katika ujinga.

:12

Wanauliza: Ni lini hiyo siku ya malipo?

:13

Hiyo ni siku watakayo adhibiwa Motoni.

:14

Onjeni adhabu yenu! Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyahimiza.

:15

Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na chemchem.

:16

Wanapokea aliyo wapa Mola wao Mlezi. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema.

:17

Walikuwa wakilala kidogo tu usiku.

:18

Na kabla ya alfajiri wakiomba maghfira.

:19

Na katika mali yao ipo haki ya mwenye kuomba na asiye omba.

:20

Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini.

:21

Na pia katika nafsi zenu - Je! Hamwoni?

:22

Na katika mbingu ziko riziki zenu na mliyo ahidiwa.

:23

Basi naapa kwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo kweli kuwa nyinyi mnasema.

:24

Je! Imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanao hishimiwa?

:25

Walipo ingia kwake wakasema: Salama! Na yeye akasema: Salama! Nyinyi ni watu nisio kujueni.

:26

Akenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliye nona.

:27

Akawakaribisha, akasema: Mbona hamli?

:28

Akahisi kuwaogopa katika nafsi yake. Wakasema: Usiwe na khofu, nao wakambashiria kupata kijana mwenye ilimu.

:29

Ndipo mkewe akawaelekea, na huku anasema na akijipiga usoni kwa mastaajabu, na kusema: Mimi ni kikongwe na tasa!

:30

Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyo sema Mola wako Mlezi. Hakika Yeye ni Mwenye hikima na Mwenye kujua.

:31

AKASEMA: Basi ujumbe wenu ni nini, enyi mlio tumwa?

:32

Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa watu wakosefu,

:33

Tuwatupie mawe ya udongo,

:34

Yaliyo tiwa alama kutoka kwa Mola wako Mlezi kwa ajili ya wanao pindukia mipaka.

:35

Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walio amini.

:36

Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu!

:37

Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanao iogopa adhabu chungu.

:38

Na katika khabari za Musa, tulipo mtuma kwa Firauni na hoja wazi.

:39

Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake na akasema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu!

:40

Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa.

:41

Na katika khabari za A'di tulipo wapelekea upepo wa kukata uzazi.

:42

Haukuacha chochote ulicho kifikia ila ulikifanya kama kilio nyambuka.

:43

Na katika khabari za Thamudi walipo ambiwa: Jifurahisheni kwa muda mdogo tu.

:44

Wakaasi amri ya Mola wao Mlezi. Basi uliwanyakua moto wa radi nao wanaona.

:45

Basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea.

:46

Na kaumu ya Nuhu hapo mbele. Hakika hao walikuwa watu wapotovu.

:47

Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio twenye uwezo wa kuzitanua.

:48

Na ardhi tumeitandaza; basi watandazaji wazuri namna gani Sisi!

:49

Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie.

:50

Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

:51

Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

:52

Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu.

:53

Je! Wameambizana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi.

:54

Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi.

:55

Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini.

:56

Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi.

:57

Na sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe.

:58

Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti.

:59

Hakika walio dhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao. Basi wasinihimize.

:60

Ole wao walio ikanusha siku yao waliyo ahidiwa.