Maktaba yote ya Kiislamu

50 - The Letter "Qaf" - Qāf

:1

Qaaf. Naapa kwa Qur'ani tukufu!

:2

Bali wanastaajabu kwamba amewafikia mwonyaji kutoka miongoni mwao, na wakasema makafiri: Hili ni jambo la ajabu!

:3

Ati tukifa na tukawa udongo...? Kurejea huko kuko mbali!

:4

Hakika Sisi tunajua kiasi cha kila kinacho punguzwa na ardhi kutokana nao. Na kwetu kipo Kitabu kinacho hifadhi yote.

:5

Lakini waliikanusha Haki ilipo wajia; kwa hivyo wamo katika mambo ya mkorogo.

:6

Je! Hawaangalii mbingu zilizo juu yao! Vipi tulivyo zijenga, na tukazipamba. Wala hazina nyufa.

:7

Na ardhi tumeitandaza na tukaiwekea milima, na tukaiotesha mimea mizuri ya kila namna.

:8

Yawe haya ni kifumbua macho na ukumbusho kwa kila mja mwenye kuelekea.

:9

Na tumeteremsha kutoka mbinguni maji yaliyo barikiwa, na kwa hayo tukaotesha mabustani na nafaka za kuvunwa.

:10

Na mitende mirefu yenye makole yaliyo zaa kwa wingi,

:11

Ili iwe ni riziki kwa waja wangu. Na tukaifufua kwa maji nchi iliyo kuwa imekufa. Kama hivyo ndivyo utakavyo kuwa ufufuaji.

:12

Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuhu na wakaazi wa Rassi na Thamudi.

:13

Na A'di na Firauni na kaumu ya Lut'i.

:14

Na wakaazi wa Machakani, na watu wa Tubbaa'. Wote hao waliwakanusha Mitume, kwa hivyo onyo likathibitika juu yao.

:15

Kwani tulichoka kwa kuumba mara ya kwanza. Bali wao wamo katika shaka tu juu ya umbo jipya.

:16

Na hakika tumemuumba mtu, nasi tunayajua yanayo mpitikia katika nafsi yake. Na Sisi tuko karibu naye kuliko mshipa wa shingoni mwake.

:17

Wanapo pokea wapokeaji wawili, wanao kaa kuliani na kushotoni.

:18

Hatamki neno ila karibu yake yupo mwangalizi tayari.

:19

Na uchungu wa kutoka roho utamjia kwa haki. Hayo ndiyo uliyo kuwa ukiyakimbia.

:20

Na litapulizwa baragumu. Hiyo ndiyo Siku ya Miadi.

:21

Na kila nafsi itakuja na pamoja nayo mchungaji na shahidi.

:22

(Aambiwe): Kwa hakika ulikuwa umeghafilika na haya; basi leo tumekuondolea pazia lako, na kwa hivyo kuona kwako leo ni kukali.

:23

Na mwenzake atasema: Huyu niliye naye mimi kesha tayarishwa.

:24

Mtupeni katika Jahannamu kila kafiri mwenye inda,

:25

Akatazaye kheri, arukaye mipaka, mwenye kutia shaka,

:26

Aliye weka mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Basi mtupeni katika adhabu kali.

:27

Mwenzake aseme: Ee Mola wetu Mlezi! Sikumpoteza mimi, bali yeye mwenyewe alikuwa katika upotovu wa mbali.

:28

(Mwenyezi Mungu) aseme: Msigombane mbele yangu. Nilikuleteeni mbele onyo langu.

:29

Mbele yangu haibadilishwi kauli, wala Mimi siwadhulumu waja wangu.

:30

Siku tutapo iambia Jahannamu: Je! Umejaa? Nayo itasema: Je! Kuna ziada?

:31

Na Pepo italetwa karibu kwa ajili ya wachamngu, haitakuwa mbali.

:32

Haya ndiyo mnayo ahidiwa kwa kila mwenye kurejea kwa Mwenyezi Mungu na akajilinda.

:33

Mwenye kumwogopa Mwingi wa Rehema hali kuwa hamwoni, na akaja kwa moyo ulio elekea-

:34

(Ataambiwa) ingieni kwa salama. Hiyo ndiyo siku ya daima dawamu.

:35

Humo watapata wakitakacho, na kwetu yako ya ziada.

:36

Na kaumu ngapi tuliziangamiza kabla yao walio kuwa na nguvu zaidi kuliko hawa! Nao walitanga tanga katika nchi nyingi. Je! Walipata pa kukimbilia?

:37

Hakika katika hayo upo ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye yupo anashuhudia.

:38

Na bila ya shaka Sisi tumeziumba mbingu na ardhi na vilio baina yao mnamo siku sita; na wala hayakutugusa machofu.

:39

Basi vumilia kwa hayo wasemayo, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi kabla ya kuchomoza jua na kabla ya kuchwa.

:40

Na katika usiku pia mtakase, na baada ya kusujudu.

:41

Na sikiliza siku atapo nadi mwenye kunadi kutoka pahala karibu.

:42

Siku watakapo sikia ukelele wa haki. Hiyo ndiyo siku ya kufufuka.

:43

Hakika Sisi tunahuisha na tunafisha, na kwetu Sisi ndio marejeo.

:44

Siku itapo wapasukia ardhi mbio mbio! Mkusanyo huo kwetu ni mwepesi.

:45

Sisi tunajua kabisa wayasemayo. Wala wewe si mwenye kuwatawalia kwa ujabari. Basi mkumbushe kwa Qur'ani anaye liogopa onyo.