Maktaba yote ya Kiislamu

52 - The Mount - Aţ-Ţūr

:1

Naapa kwa mlima wa T'ur,

:2

Na Kitabu kilicho andikwa

:3

Katika ngozi iliyo kunjuliwa,

:4

Na kwa Nyumba iliyo jengwa,

:5

Na kwa dari iliyo nyanyuliwa,

:6

Na kwa bahari iliyo jazwa,

:7

Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi hapana shaka itatokea.

:8

Hapana wa kuizuia.

:9

Siku zitakapo tikisika mbingu kwa mtikiso,

:10

Na milima iwe inakwenda kwa mwendo mkubwa.

:11

Basi ole wao siku hiyo hao wanao kadhibisha,

:12

Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi.

:13

Siku watapo sukumwa kwenye Moto kwa msukumo wa nguvu,

:14

(Waambiwe): Huu ndio ule Moto mlio kuwa mkiukanusha!

:15

Je! Huu ni uchawi, au hamwoni tu?

:16

Uingieni, mkistahamili au msistahamili - ni mamoja kwenu. Hakika mnalipwa kwa mliyo kuwa mkiyatenda.

:17

Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na neema,

:18

Wakifurahi kwa yale aliyo wapa Mola wao Mlezi. Na Mola wao Mlezi atawalinda na adhabu ya Motoni.

:19

Kuleni na kunyweni kwa raha kabisa kwa sababu ya mliyo kuwa mkiyatenda.

:20

Watakuwa wameegemea juu ya viti vya enzi vilivyo pangwa kwa safu. Na tutawaoza mahuru-l-aini.

:21

Na walio amini na dhuriya zao wakawafuata kwa Imani tutawakutanisha nao dhuriya zao, na wala hatutawapunja hata kidogo katika vitendo vyao. Kila mtu lazima atapata alicho kichuma.

:22

Na tutawapa matunda, na nyama kama watavyo penda.

:23

Watapeana humo bilauri zisio na vinywaji vya kuleta maneno ya upuuzi wala dhambi.

:24

Iwe wanawapitia watumishi wao kama kwamba ni lulu zilizomo katika chaza.

:25

Wataelekeana wakiulizana.

:26

Waseme: Tulikuwa zamani pamoja na ahali zetu tukiogopa;

:27

Basi Mwenyezi Mungu akatufanyia hisani na akatulinda na adhabu ya upepo wa Moto.

:28

Hakika sisi zamani tulikuwa tukimwomba Yeye tu. Hakika Yeye ndiye Mwema Mwenye kurehemu.

:29

Basi kumbusha! Kwani wewe, kwa neema ya Mola wako Mlezi, si kuhani wala mwendawazimu.

:30

Au wanasema: Huyu ni mtunga mashairi, tunamtarajia kupatilizwa na dahari.

:31

Sema: Tarajieni, na mimi pia ni pamoja nanyi katika kutarajia.

:32

Au hizo akili zao ndio zinawaamrisha haya, au wao basi ni watu majeuri tu?

:33

Au ndio wanasema: Ameitunga hii! Bali basi tu hawaamini!

:34

Basi nawalete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli.

:35

Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji?

:36

Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana na yakini.

:37

Au wanazo khazina za Mola wako Mlezi au wao ndio wenye madaraka?

:38

Au wanazo ngazi za kusikilizia? Basi huyo msikilizaji wao na alete hoja ilio wazi!

:39

Au Yeye Mwenyezi Mungu ana wasichana, na nyinyi ndio mna wavulana?

:40

Au wewe unawaomba ujira, na kwa hivyo ndio wanaelemewa na uzito wa gharama?

:41

Au wanayo ilimu ya ghaibu, nao wameandika?

:42

Au wanataka kufanya vitimbi tu? Lakini hao walio kufuru ndio watakao tegeka.

:43

Au wanae mungu asiye kuwa Mwenyezi Mungu? Subhanallah! Ametaksika Mwenyezi Mungu na hao wanao washirikisha naye.

:44

Na hata wange ona pande linatoka mbinguni linaanguka wange sema: Ni mawingu yaliyo bebana.

:45

Basi waache mpaka wakutane na siku yao watakapo hilikishwa.

:46

Siku ambayo hila zao hazitawafaa hata kidogo, wala wao hawatanusuriwa.

:47

Na hakika walio dhulumu watapata adhabu nyengine isiyo kuwa hii, lakini wengi wao hawajui.

:48

Na ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi. Kwani wewe hakika uko mbele ya macho yetu, na mtakase kwa kumsifu Mola wako Mlezi unapo simama,

:49

Na usiku pia mtakase, na zinapo kuchwa nyota.