Maktaba yote ya Kiislamu

56 - The Inevitable - Al-Wāqi`ah

:1

Litakapo tukia hilo Tukio

:2

Hapana cha kukanusha kutukia kwake.

:3

Literemshalo linyanyualo,

:4

Itakapo tikiswa ardhi kwa mtikiso,

:5

Na milima itapo sagwasagwa,

:6

Iwe mavumbi yanayo peperushwa,

:7

Na nyinyi mtakuwa namna tatu:-

:8

Basi watakuwepo wa kuliani; je, ni wepi wa kuliani?

:9

Na wa kushotoni; je, ni wepi wa kushotoni?

:10

Na wa mbele watakuwa mbele.

:11

Hao ndio watakao karibishwa

:12

Katika Bustani zenye neema.

:13

Fungu kubwa katika wa mwanzo,

:14

Na wachache katika wa mwisho.

:15

Watakuwa juu ya viti vya fakhari vilivyo tonewa.

:16

Wakiviegemea wakielekeana.

:17

Wakitumikiwa na wavulana wa ujana wa milele,

:18

Kwa vikombe na mabirika na bilauri za vinywaji kutoka chemchem safi.

:19

Hawataumwa kichwa kwa vinywaji hivyo wala hawatoleweshwa.

:20

Na matunda wayapendayo,

:21

Na nyama za ndege kama wanavyo tamani.

:22

Na Mahurulaini,

:23

Walio kama mfano wa lulu zilio hifadhiwa.

:24

Ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda.

:25

Humo hawatasikia porojo wala maneno ya dhambi,

:26

Isipo kuwa maneno ya Salama, Salama.

:27

Na wale wa mkono wa kulia, ni yepi yatakuwa ya wa kuliani?

:28

Katika mikunazi isiyo na miba,

:29

Na migomba iliyo pangiliwa,

:30

Na kivuli kilicho tanda,

:31

Na maji yanayo miminika,

:32

Na matunda mengi,

:33

Hayatindikii wala hayakatazwi,

:34

Na matandiko yaliyo nyanyuliwa.

:35

Hakika Sisi tutawaumba (Mahurulaini) upya,

:36

Na tutawafanya vijana,

:37

Wanapendana na waume zao, hirimu moja.

:38

Kwa ajili ya watu wa kuliani.

:39

Fungu kubwa katika wa mwanzo,

:40

Na fungu kubwa katika wa mwisho.

:41

Na watu wa kushotoni; je ni yepi ya wa kushotoni?

:42

Katika upepo wa moto, na maji yanayo chemka,

:43

Na kivuli cha moshi mweusi,

:44

Si cha kuburudisha wala kustarehesha.

:45

Hakika hao walikuwa kabla ya haya wakiishi maisha ya anasa.

:46

Na walikuwa wakishikilia kufanya madhambi makubwa,

:47

Na walikuwa wakisema: Tutakapo kufa na tukawa udongo na mafupa, ati ndio tutafufuliwa?

:48

Au baba zetu wa zamani?

:49

Sema: Hakika wa zamani na wa mwisho

:50

Bila ya shaka watakusanywa kwa wakati wa siku maalumu.

:51

Kisha nyinyi, mlio potea, mnao kanusha,

:52

Kwa yakini mtakula mti wa Zaqqumu.

:53

Na kwa mti huo mtajaza matumbo.

:54

Na juu yake mtakunywa maji yanayo chemka.

:55

Tena mtakunywa kama wanavyo kunywa ngamia wenye kiu.

:56

Hiyo ndiyo karamu yao Siku ya Malipo.

:57

Sisi tumekuumbeni; basi hamsadiki?

:58

Je! Mnaiona mbegu ya uzazi mnayo idondokeza?

:59

Je! Mnaiumba nyinyi, au ni Sisi ndio Waumbaji?

:60

Sisi tumekuwekeeni mauti; na wala Sisi hatushindwi

:61

Kuwaleta wengine badala yenu na kukuumbeni nyinyi kwa umbo msilo lijua.

:62

Na bila ya shaka mlikwisha jua umbo la kwanza, basi kwa nini hamkumbuki?

:63

Je! Mnaona makulima mnayo yapanda?

:64

Je! Ni nyinyi mnayo yaotesha au ni Sisi ndio wenye kuotesha?

:65

Tungeli taka tungeli yafanya yakawa mapepe, mkabaki mnastaajabu,

:66

Mkisema: Hakika sisi tumegharimika;

:67

Bali sisi tumenyimwa.

:68

Je! Mnayaona maji mnayo yanywa?

:69

Je! Ni nyinyi mnayo yateremsha kutoka mawinguni au ni Sisi ndio wenye kuyateremsha?

:70

Tungeli penda tungeli yafanya ya chumvi. Basi mbona hamshukuru?

:71

Je! Mnauona moto mnao uwasha?

:72

Ni nyinyi mlio uumba mti wake au Sisi ndio Waumbaji?

:73

Sisi tumeufanya uwe ni ukumbusho na manufaa kwa walioko nyikani.

:74

Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkuu.

:75

Basi naapa kwa maanguko ya nyota,

:76

Na hakika bila ya shaka hichi ni kiapo kikubwa, laiti mngeli jua!

:77

Hakika hii bila ya shaka ni Qur'ani Tukufu,

:78

Katika Kitabu kilicho hifadhiwa.

:79

Hapana akigusaye ila walio takaswa.

:80

Ni uteremsho unao toka kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:81

Ni maneno haya ndiyo nyinyi mnayapuuza?

:82

Na badala ya kushukuru kwa riziki yenu mnafanya kuwa mnakadhibisha?

:83

Yawaje basi itakapo fika roho kwenye koo,

:84

Na nyinyi wakati huo mnatazama!

:85

Na Sisi tuko karibu zaidi naye kuliko nyinyi.

:86

Na lau kuwa nyinyi hamumo katika mamlaka yangu,

:87

Kwanini hamuirudishi hiyo roho, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

:88

Basi akiwa miongoni mwa walio karibishwa,

:89

Basi ni raha, na manukato, na Bustani zenye neema.

:90

Na akiwa katika watu wa upande wa kulia,

:91

Basi ni Salamu kwako uliye miongoni mwa watu wa upande wa kulia.

:92

Na ama akiwa katika walio kadhibisha wapotovu,

:93

Basi karamu yake ni maji yanayo chemka,

:94

Na kutiwa Motoni.

:95

Hakika hii ndiyo haki yenye yakini.

:96

Basi litakase jina la Mola wako Mlezi aliye Mkubwa.