Maktaba yote ya Kiislamu

54 - The Moon - Al-Qamar

:1

Saa imekaribia, na mwezi umepasuka!

:2

Na wakiona Ishara hugeuka upande na husema: Huu uchawi tu unazidi kuendelea.

:3

Na wamekanusha na wamefuata matamanio yao. Na kila jambo ni lenye kuthibiti.

:4

Na bila ya shaka zimewajia khabari zenye makaripio.

:5

Hikima kaamili; lakini maonyo hayafai kitu!

:6

Basi jiepushe nao. Siku atakapo ita mwitaji kuliendea jambo linalo chusha;

:7

Macho yao yatainama; watatoka makaburini kama nzige walio tawanyika,

:8

Wanamkimbilia mwitaji, na makafiri wanasema: Hii ni siku ngumu.

:9

Kabla yao kaumu ya Nuhu walikanusha; wakamkanusha mja wetu, na wakasema ni mwendawazimu, na akakaripiwa.

:10

Basi akamwomba Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika mimi nimeshindwa, basi ninusuru!

:11

Basi tukaifungua milango ya mbingu kwa maji yanayo miminika.

:12

Na tukazipasua ardhi kwa chemchem, yakakutana maji kwa jambo lilio kadiriwa.

:13

Na tukamchukua kwenye safina ya mbao na kamba.

:14

Ikawa inakwenda kwa nadhari yetu, kuwa ni malipo kwa alivyo kuwa amekanushwa.

:15

Na bila ya shaka tuliiacha iwe ni Ishara. Lakini je, yupo anaye kumbuka?

:16

Basi ilikuwaje adhabu yangu, na maonyo yangu.

:17

Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kufahamika. Lakini yupo anaye kumbuka?

:18

Kina A'di walikanusha. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?

:19

Hakika Sisi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku korofi mfululizo,

:20

Ukiwang'oa watu kama vigogo vya mitende vilio ng'olewa.

:21

Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?

:22

Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani nyepesi kufahamika; lakini yupo anaye kumbuka?

:23

Thamudi waliwakanusha Waonyaji.

:24

Wakasema: Ati tumfuate binaadamu mmoja katika sisi? Basi hivyo sisi tutakuwa katika upotofu na kichaa!

:25

Ni yeye tu aliye teremshiwa huo ukumbusho kati yetu sote? Bali huyu ni mwongo mwenye kiburi!

:26

Kesho watajua ni nani huyo mwongo mwenye kiburi.

:27

Hakika Sisi tutawapelekea ngamia jike ili kuwajaribu, basi watazame tu na ustahamili.

:28

Na waambie kwamba maji yatagawanywa baina yao; kila sehemu ya maji itahudhuriwa na aliye khusika.

:29

Basi wakamwita mtu wao akaja akamchinja.

:30

Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu!

:31

Hakika Sisi tuliwapelekea ukelele mmoja tu, wakawa kama mabuwa ya kujengea uwa.

:32

Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur'ani iwe nyepesi kwa kukumbuka, lakini yupo akumbukaye?

:33

Kaumu Lut'i nao waliwakadhibisha Waonyaji.

:34

Hakika Sisi tukawapelekea kimbunga cha vijiwe, isipo kuwa wafuasi wa Lut'i. Hao tuliwaokoa karibu na alfajiri.

:35

Kwa neema inayo toka kwetu. Hivyo ndivyo tumlipavyo anaye shukuru.

:36

Na hakika yeye aliwaonya adhabu yetu; lakini wao waliyatilia shaka hayo maonyo.

:37

Na walimtaka awape wageni wake. Tukayapofua macho yao, na tukawaambia: Onjeni basi adhabu na maonyo yangu!

:38

Na iliwafikia wakati wa asubuhi adhabu yangu ya kuendelea.

:39

Basi onjeni adhabu na maonyo yangu!

:40

Na hakika tumeisahilisha Qur'ani kuikumbuka. Lakini yupo anaye kumbuka?

:41

Na Waonyaji waliwafikia watu wa Firauni.

:42

Walizikadhibisha Ishara zetu zote, nasi tukawashika kama anavyo shika Mwenye nguvu Mwenye uweza.

:43

Je! Makafiri wenu ni bora kuliko hao, au yameandikwa vitabuni kuwa nyinyi hamtiwi makosani?

:44

Au ndio wanasema: Sisi ni wengi tutashinda tu.

:45

Wingi wao huu utashindwa, na wao watasukumwa nyuma.

:46

Bali Saa ya Kiyama ndio miadi yao, na Saa hiyo ni nzito zaidi na chungu zaidi.

:47

Hakika wakosefu wamo katika upotofu na wazimu.

:48

Siku watakapo kokotwa Motoni kifudifudi waambiwe: Onjeni mguso wa Jahannamu!

:49

Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo.

:50

Na amri yetu haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho.

:51

Na bila ya shaka tumekwisha waangamiza wenzenu. Lakini yupo anaye kumbuka?

:52

Na kila jambo walilo lifanya limo vitabuni.

:53

Na kila kidogo na kikubwa kimeandikwa.

:54

Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na mito.

:55

Katika makalio ya haki kwa Mfalme Mwenye uweza.