Maktaba yote ya Kiislamu

37 - Those who set the Ranks - Aş-Şāffāt

:1

Naapa kwa wanao jipanga kwa safu.

:2

Na kwa wenye kukataza mabaya.

:3

Na kwa wenye kusoma Ukumbusho.

:4

Hakika Mungu wenu bila ya shaka ni Mmoja.

:5

Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na yaliyomo kati yao, na ni Mola Mlezi wa mashariki zote.

:6

Hakika Sisi tumeipamba mbingu ya karibu kwa pambo la nyota.

:7

Na kulinda na kila shet'ani a'si.

:8

Wasiweze kuwasikiliza viumbe watukufu. Na wanafukuzwa huko kila upande.

:9

Wakifurushwa. Na wanayo adhabu ya kudumu.

:10

Isipo kuwa anaye nyakua kitu kidogo, na mara humfwatia kimondo kinacho ng'ara.

:11

Hebu waulize: Je! Wao ni wenye umbo gumu zaidi au hao wengine tulio waumba. Hakika Sisi tuliwaumba wao kwa udongo unao nata.

:12

Bali unastaajabu, na wao wanafanya maskhara.

:13

Na wanapo kumbushwa hawakumbuki.

:14

Na wanapo ona Ishara, wanafanya maskhara.

:15

Na husema: Haya si chochote ila ni uchawi tu ulio dhaahiri.

:16

Ati tukisha kufa na tukawa udongo na mifupa ndio kweli tutafufuliwa?

:17

Hata baba zetu wa zamani?

:18

Sema: Naam! Hali nanyi ni madhalili.

:19

Huko utapigwa ukelele mmoja tu! Na hapo ndio wataona!

:20

Watasema: Ole wetu! Hii ndiyo Siku ya Malipo.

:21

Hii ndiyo Siku ya Hukumu mliyo kuwa mkiikadhibisha.

:22

Wakusanyeni walio dhulumu, na wake zao, na hao walio kuwa wakiwaabudu -

:23

Badala ya Mwenyezi Mungu. Waongozeni njia ya Jahannamu!

:24

Na wasimamisheni. Hakika hao watasailiwa:

:25

Mna nini? Mbona hamsaidiani?

:26

Bali hii leo, watasalimu amri.

:27

Watakabiliana wao kwa wao kuulizana.

:28

Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kulia.

:29

Watasema (wakubwa): Bali nyinyi wenyewe hamkuwa Waumini.

:30

Sisi hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi wenyewe mlikuwa wapotovu.

:31

Basi hukumu ya Mola wetu Mlezi imekwisha tuthibitikia. Hakika bila ya shaka tutaonja tu adhabu.

:32

Tulikupotezeni kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu.

:33

Basi wao kwa hakika siku hiyo watashirikiana katika adhabu pamoja.

:34

Hivyo ndivyo tutakavyo wafanyia wakosefu.

:35

Wao walipo kuwa wakiambiwa La ilaha illa 'Llahu Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu tu, wakijivuna.

:36

Na wakisema: Hivyo sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu?

:37

Bali huyu amekuja kwa Haki, na amewasadikisha Mitume.

:38

Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu.

:39

Wala hamlipwi ila hayo mliyo kuwa mkiyafanya.

:40

Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio khitariwa.

:41

Hao ndio watakao pata riziki maalumu,

:42

Matunda, nao watahishimiwa.

:43

Katika Bustani za neema.

:44

Wako juu ya viti wamekabiliana.

:45

Wanazungushiwa kikombe chenye kinywaji cha chemchem

:46

Kinywaji cheupe, kitamu kwa wanywao.

:47

Hakina madhara, wala hakiwaleweshi.

:48

Na watakuwa nao wanawake wenye macho ya staha mazuri.

:49

Hao wanawake kama mayai yaliyo hifadhika.

:50

Waingie kuulizana wenyewe kwa wenyewe.

:51

Aseme msemaji mmoja miongoni mwao: Hakika mimi nalikuwa na rafiki

:52

Aliye kuwa akinambia: Hivyo wewe ni katika wanao sadiki

:53

Ati tukisha kufa tukawa udongo na mafupa, ndio tutalipwa na kuhisabiwa?

:54

Atasema: Je! Nyie mnawaona?

:55

Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.

:56

Atasema: Wallahi! Ulikaribia kunipoteza.

:57

Na lau kuwa si neema ya Mola wangu Mlezi bila ya shaka ningeli kuwa miongoni mwa walio hudhurishwa.

:58

Je! Sisi hatutakufa,

:59

Isipo kuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa.

:60

Hakika huku bila ya shaka ndiko kufuzu kukubwa.

:61

Kwa mfano wa haya nawatende watendao.

:62

Je! Kukaribishwa hivi si ndio bora, au mti wa Zaqqum?

:63

Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni mateso kwa walio dhulumu.

:64

Hakika huo ni mti unao toka katikati ya Jahannamu.

:65

Mashada ya matunda yake kama kwamba vichwa vya mashet'ani.

:66

Basi hakika bila ya shaka hao watayala hayo, na wajaze matumbo.

:67

Kisha juu yake wanyweshwe mchanganyo wa maji yamoto yaliyo chemka.

:68

Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu.

:69

Hakika waliwakuta baba zao wamepotea.

:70

Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.

:71

Na bila ya shaka walikwisha potea kabla yao wengi wa watu wa zamani.

:72

Na Sisi hakika tuliwapelekea waonyaji.

:73

Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa walio onywa.

:74

Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio khitariwa.

:75

Na hakika Nuhu alitwita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.

:76

Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.

:77

Na tuliwajaalia dhuriya zake ndio wenye kubakia.

:78

Na tukamwachia (sifa njema) kwa walio kuja baadaye.

:79

Iwe salama kwa Nuhu ulimwenguni kote!

:80

Kwa hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao fanya mema.

:81

Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini.

:82

Kisha tukawazamisha wale wengine.

:83

Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake,

:84

Alipo mjia Mola wake Mlezi kwa moyo mzima.

:85

Alimwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini?

:86

Kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?

:87

Mnamdhania nini Mola Mlezi wa walimwengu wote?

:88

Kisha akapiga jicho kutazama nyota.

:89

Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!

:90

Nao wakamwacha, wakampa kisogo.

:91

Basi akaiendea miungu yao kwa siri, akaiambia: Mbona hamli?

:92

Mna nini hata hamsemi?

:93

Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kulia.

:94

Basi wakamjia upesi upesi.

:95

Akasema: Hivyo mnaviabudu vitu mnavyo vichonga wenyewe?

:96

Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliye kuumbeni nyinyi na hivyo mnavyo vifanya!

:97

Wakasema: Mjengeeni jengo, na kisha mtupeni motoni humo!

:98

Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini.

:99

Na akasema: Hakika mimi nahama, nakwenda kwa Mola wangu Mlezi; Yeye ataniongoa.

:100

Ewe Mola wangu Mlezi! Nitunukie aliye miongoni mwa watenda mema.

:101

Basi tukambashiria mwana aliye mpole.

:102

Basi alipo fika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, alimwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja. Basi angalia wewe, waonaje? Akasema: Ewe baba yangu! Tenda unavyo amrishwa, utanikuta mimi, Inshallah, katika wanao subiri.

:103

Basi wote wawili walipo jisalimisha, na akamlaza juu ya kipaji.

:104

Tulimwita: Ewe Ibrahim!

:105

Umekwisha itimiliza ndoto. Hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao tenda mema.

:106

Hakika haya ni majaribio yaliyo dhaahiri.

:107

Basi tukamtolea fidia kwa dhabihu mtukufu.

:108

Na tukamwachia (sifa njema) kwa watu walio kuja baadaye.

:109

Iwe salama kwa Ibrahim!

:110

Hivi ndivyo tunavyo walipa wanao fanya mema.

:111

Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini.

:112

Na tukambashiria kuzaliwa Is-haqa, naye ni Nabii miongoni mwa watu wema.

:113

Na tukambarikia yeye na Is-haqa. Na miongoni mwa dhuriya zao walitokea wema na wenye kudhulumu nafsi zao waziwazi.

:114

Na kwa hakika tuliwafanyia hisani Musa na Haruni.

:115

Na tukawaokoa wao na watu wao kutokana na dhiki kubwa.

:116

Na tukawanusuru; na wakawa wao ndio wenye kushinda.

:117

Na tukawapa wawili hao Kitabu kinacho bainisha.

:118

Na tukawaongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka.

:119

Na tukawaachia (sifa njema) katika watu walio kuja baadaye.

:120

Iwe salama kwa Musa na Haruni!

:121

Hakika hivyo ndivyo tunavyo walipa walio wema.

:122

Hakika wawili hao ni katika waja wetu walio amini.

:123

Na hakika Ilyas bila ya shaka alikuwa miongoni mwa Mitume.

:124

Alipo waambia watu wake: Hamwogopi?

:125

Mnamwomba Baa'li na mnamwacha Mbora wa waumbaji,

:126

Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa baba zenu wa zamani?

:127

Wakamkadhibisha. Basi kwa hakika watahudhurishwa;

:128

Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio safishwa.

:129

Na tumemwachia (sifa nzuri) kwa walio kuja baadaye.

:130

Iwe salama kwa Ilyas.

:131

Hakika hivyo ndivyo tunavyo walipa walio wema.

:132

Hakika yeye ni katika waja wetu walio amini.

:133

Na hakika Lut'i bila ya shaka ni miongoni mwa Mitume.

:134

Tulipo mwokoa yeye na ahali zake wote,

:135

Isipo kuwa mwanamke mkongwe katika wale walio bakia nyuma.

:136

Kisha tukawaangamiza wale wengineo.

:137

Na hakika nyinyi mnawapitia wakati wa asubuhi,

:138

Na usiku. Basi je! Hamyatii akilini?

:139

Na hakika Yunus alikuwa miongoni mwa Mitume.

:140

Alipo kimbia katika jahazi lilio sheheni.

:141

Akaingia katika kupigiwa kura, na akawa katika walio shindwa.

:142

Samaki akammeza hali ya kuwa ni mwenye kulaumiwa.

:143

Na ingeli kuwa hakuwa katika wanao mtakasa Mwenyezi Mungu,

:144

Bila ya shaka angeli kaa ndani yake mpaka siku ya kufufuliwa.

:145

Lakini tulimtupa ufukweni patupu, hali yu mgonjwa.

:146

Na tukauotesha juu yake mmea wa kabila ya mung'unye.

:147

Na tulimtuma kwa watu laki moja au zaidi.

:148

Basi wakaamini, na tukawastarehesha kwa muda.

:149

Basi waulize: Ati Mola wako Mlezi ndiye mwenye watoto wa kike, na wao wanao watoto wa kiume?

:150

Au tumewaumba Malaika kuwa ni wanawake, na wao wakashuhudia?

:151

Ati ni kwa uzushi wao ndio wanasema:

:152

Mwenyezi Mungu amezaa! Ama hakika bila ya shaka hao ni waongo!

:153

Ati amekhiari watoto wa kike kuliko wanaume?

:154

Mna nini? Mnahukumu vipi nyinyi?

:155

Hamkumbuki?

:156

Au mnayo hoja iliyo wazi?

:157

Basi leteni Kitabu chenu kama mnasema kweli.

:158

Na wameweka makhusiano ya nasaba baina yake na majini; na majini wamekwisha jua bila ya shaka kuwa wao watahudhurishwa.

:159

Subhana 'Llah Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayo msingizia.

:160

Isipo kuwa waja wa Mwenyezi Mungu walio safishwa.

:161

Basi hakika nyinyi na mnao waabudu

:162

Hamwezi kuwapoteza

:163

Isipo kuwa yule atakaye ingia Motoni.

:164

Na hapana katika sisi ila anapo mahali pake maalumu.

:165

Na hakika bila ya shaka sisi ndio wajipangao safu.

:166

Na hakika sisi ndio wenye kusabihi kutakasa.

:167

Na walikuwapo walio kuwa wakisema:

:168

Tungeli kuwa na Ukumbusho kama wa watu wa zamani,

:169

Bila ya shaka tungeli kuwa ni waja wa Mwenyezi Mungu wenye ikhlasi.

:170

Lakini waliukataa. Basi watakuja jua.

:171

Na bila ya shaka neno letu lilikwisha tangulia kwa waja wetu walio tumwa.

:172

Ya kuwa wao bila ya shaka ndio watakao nusuriwa.

:173

Na kwamba jeshi letu ndilo litakalo shinda.

:174

Basi waachilie mbali kwa muda.

:175

Na watazame, nao wataona.

:176

Je! Wanaihimiza adhabu yetu?

:177

Basi itakapo shuka uwanjani kwao, itakuwa asubuhi mbaya kwa walio onywa.

:178

Na waache kwa muda.

:179

Na tazama, na wao wataona.

:180

Subhana Rabbi'l'Izzat Ametakasika Mola Mlezi Mwenye enzi na yale wanayo mzulia.

:181

Na Salamu juu ya Mitume.

:182

Na sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.