Maktaba yote ya Kiislamu

26 - The Poets - Ash-Shu`arā

:1

T'aa Siin Miim. (T'. S. M.)

:2

Hizi ni Aya za Kitabu kinacho bainisha.

:3

Huenda labda ukajikera nafsi yako kwa kuwa hawawi Waumini.

:4

Tunge penda tungeli wateremshia kutoka mbinguni Ishara zikanyenyekea shingo zao.

:5

Wala hauwafikii ukumbusho mpya kutoka kwa Arrahman ila wao hujitenga nao.

:6

Kwa yakini wamekanusha; kwa hivyo zitakuja wafikia khabari za yale waliyo kuwa wakiyafanyia mzaha.

:7

Je! Hawakuiona ardhi, mimea mingapi tumeiotesha humo, ya kila namna nzuri?

:8

Hakika katika haya zipo Ishara. Lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

:9

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:10

Na Mola wako Mlezi, alipo mwita Musa, akamwambia: Fika kwa watu madhaalimu,

:11

Watu wa Firauni. Hawaogopi?

:12

Akasema: Hakika mimi nachelea wasinikanushe.

:13

Na kifua changu kina dhiki, na ulimi wangu haukunjuki vyema. Basi mtumie ujumbe Harun.

:14

Na wao wana kisasi juu yangu, kwa hivyo naogopa wasije kuniuwa.

:15

Akasema: Siyo hivyo kabisa! Nendeni na miujiza yetu. Hakika Sisi tu pamoja nanyi, tunasikiliza.

:16

Basi mfikieni Firauni na mwambieni: Hakika sisi ni Mitume wa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:17

Waachilie Wana wa Israili wende nasi.

:18

(Firauni) akasema: Sisi hatukukulea wewe utotoni, na ukakaa kwetu katika umri wako miaka mingi?

:19

Na ukatenda kitendo chako ulicho tenda, nawe ukawa miongoni mwa wasio na shukrani?

:20

(Musa) akasema: Nilitenda hayo hapo nilipo kuwa miongoni mwa wale walio potea.

:21

Basi nikakukimbieni nilipo kuogopeni, tena Mola wangu Mlezi akanitunukia hukumu, na akanijaalia niwe miongoni mwa Mitume.

:22

Na hiyo ndiyo neema ya kunisumbulia, na wewe umewatia utumwani Wana wa Israili?

:23

Firauni akasema: Na nani huyo Mola Mlezi wa walimwengu wote?

:24

Akasema: Ndiye Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, na viliomo baina yao, ikiwa nyinyi ni wenye yakini.

:25

(Firauni) akawaambia walio mzunguka: Hamsikilizi?

:26

(Musa) akasema: Ndiye Mola wenu Mlezi, na Mola Mlezi wa baba zenu wa kwanza.

:27

(Firauni) akasema: Hakika huyu Mtume wenu aliye tumwa kwenu ni mwendawazimu.

:28

(Musa) akasema: Ndiye Mola Mlezi wa Mashariki na Magharibi na viliomo baina yao, ikiwa nyinyi mnatia akilini.

:29

(Firauni) akasema: Ukimfuata mungu mwengine asiye kuwa mimi, basi bila ya shaka nitakufunga gerezani.

:30

Akasema: Je! Ijapo kuwa nitakuletea kitu cha kubainisha wazi?

:31

Akasema: Kilete basi, kama wewe ni katika wasemao kweli.

:32

Basi akaitupa fimbo yake, mara ikawa nyoka wa kuonekana dhaahiri.

:33

Na akautoa mkono wake, na mara ukawa mweupe kwa watazamao.

:34

(Firauni) akawaambia waheshimiwa walio mzunguka: Hakika huyu ni mchawi mtaalamu.

:35

Anataka kukutoeni katika nchi yenu kwa uchawi wake. Basi mna shauri gani?

:36

Wakasema: Mpe muda yeye na nduguye na uwatume mijini wapigao mbiu ya mgambo.

:37

Wakuletee kila mchawi bingwa mtaalamu.

:38

Basi wakakusanywa wachawi wakati na siku maalumu.

:39

Na watu wakaambiwa: Je! Mtakusanyika?

:40

Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakao shinda.

:41

Basi walipo kuja wachawi wakamwambia Firauni: Je! Tutapata ujira tukiwa sisi ndio tulio shinda?

:42

Naam! Na hakika mtakuwa katika watu wa mbele.

:43

Musa akwaambia: Tupeni mnavyo taka kutupa.

:44

Basi wakatupa kamba zao na fimbo zao, na wakasema: Kwa nguvu za Firauni hakika sisi hapana shaka ni wenye kushinda.

:45

Musa tena akatupa fimbo yake, nayo mara ikavimeza walivyo vizua.

:46

Hapo wachawi walipinduka wakasujudu.

:47

Wakasema: Tunamuamini Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:48

Mola Mlezi wa Musa na Harun.

:49

(Firauni) akasema: Je! Mmemuamini kabla sijakuruhusuni? Bila ya shaka yeye basi ndiye mkubwa wenu aliye kufunzeni uchawi. Basi mtakuja jua! Nitakata mikono yenu na miguu yenu kwa kutafautisha. Na nitakubandikeni misalabani nyote.

:50

Wakasema: Haidhuru, kwani sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.

:51

Hakika sisi tunatumai Mola wetu Mlezi atatusamehe makosa yetu, kwa kuwa ndio wa kwanza wa kuamini.

:52

Na tulimuamrisha Musa kwa wahyi: Nenda na waja wangu wakati wa usiku. Kwa hakika mtafuatwa.

:53

Basi Firauni akawatuma mijini wapiga mbiu za mgambo.

:54

(Wakieneza): Hakika hawa ni kikundi kidogo.

:55

Nao wanatuudhi.

:56

Na sisi ni wengi, wenye kuchukua hadhari.

:57

Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem,

:58

Na makhazina, na vyeo vya hishima,

:59

Kadhaalika; na tukawarithisha hayo Wana wa Israili.

:60

Basi wakawafuata lilipo chomoza jua.

:61

Na yalipo onana majeshi mawili haya, watu wa Musa wakasema: Hakika sisi bila ya shaka tumepatikana!

:62

(Musa) akasema: Hasha! Hakika yu pamoja nami Mola wangu Mlezi. Yeye ataniongoa!

:63

Tulimletea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana, na kila sehemu ikawa kama mlima mkubwa.

:64

Na tukawajongeza hapo wale wengine.

:65

Tukawaokoa Musa na walio kuwa pamoja naye wote.

:66

Kisha tukawazamisha hao wengine.

:67

Hakika bila ya shaka katika hayo ipo Ishara; lakini wengi wao si katika wenye kuamini.

:68

Na kwa hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:69

Na wasomee khabari za Ibrahim.

:70

Alipo mwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

:71

Wakasema: Tunaabudu masanamu, daima tunayanyenyekea.

:72

Akasema: Je! Yanakusikieni mnapo yaita?

:73

Au yanakufaeni, au yanakudhuruni?

:74

Wakasema: Bali tumewakuta baba zetu wakifanya hivyo hivyo.

:75

Je! Mmewaona hawa mnao waabudu-

:76

Nyinyi na baba zenu wa zamani?

:77

Kwani hakika hao ni adui zangu, isipo kuwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:78

Ambaye ndiye aliye niumba, na Yeye ndiye ananiongoa,

:79

Na ambaye ndiye ananilisha na kuninywesha.

:80

Na ninapo ugua ni Yeye ndiye anaye niponesha.

:81

Na ambaye atanifisha, na kisha atanihuisha.

:82

Na ambaye ndiye ninaye mtumai kunisamehe makosa yangu Siku ya Malipo.

:83

Mola wangu Mlezi! Nitunukie hukumu na uniunganishe na watendao mema.

:84

Na unijaalie nitajwe kwa wema na watu watakao kuja baadaye.

:85

Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

:86

Na umsamehe baba yangu, kwani hakika alikuwa miongoni mwa wapotovu.

:87

Wala usinihizi Siku watapo fufuliwa.

:88

Siku ambayo kwamba mali hayato faa kitu wala wana.

:89

Isipo kuwa mwenye kumjia Mwenyezi Mungu na moyo safi.

:90

Na Pepo itasogezwa kwa wachamngu.

:91

Na Jahannamu itadhihirishwa kwa wapotovu.

:92

Na wataambiwa: Wako wapi mlio kuwa mkiwaabudu

:93

Badala ya Mwenyezi Mungu? Je! Wanakusaidieni, au wanajisaidia wenyewe?

:94

Basi watavurumizwa humo wao na hao wakosefu,

:95

Na majeshi ya Ibilisi yote.

:96

Watasema, na hali ya kuwa wanazozana humo:

:97

Wallahi! Kwa yakini tulikuwa katika upotovu ulio dhaahiri,

:98

Tulipo kufanyeni ni sawa na Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:99

Na hawakutupoteza ila wale wakosefu.

:100

Basi hatuna waombezi.

:101

Wala rafiki wa dhati.

:102

Laiti tungeli pata kurejea tena tungeli kuwa katika Waumini.

:103

Hakika katika haya ipo Ishara, lakini wengi wao hawakuwa wenye kuamini.

:104

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:105

Kaumu ya Nuhu waliwakadhibisha Mitume.

:106

Alipo waambia ndugu yao, Nuhu: Je! Hamchimngu?

:107

Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu.

:108

Basi Mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

:109

Na sikutakini juu yake ujira, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:110

Basi Mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

:111

Wakasema: Je! Tukuamini wewe, hali wanao kufuata ni watu wa chini?

:112

Akasema: Nayajuaje waliyo kuwa wakiyafanya?

:113

Hisabu yao haiko ila kwa Mola wao Mlezi, laiti mngeli tambua!

:114

Wala mimi si wa kuwafukuza Waumini.

:115

Mimi si cho chote ila ni Mwonyaji wa dhaahiri shaahiri.

:116

Wakasema: Ikiwa huachi, ewe Nuhu, bila ya shaka utapigwa mawe.

:117

Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika watu wangu wamenikanusha.

:118

Basi hukumu baina yangu na wao kwa hukumu yako, na uniokoe mimi na walio pamoja nami, Waumini.

:119

Kwa hivyo tukamwokoa yeye na walio kuwa pamoja naye katika marikebu iliyo sheheni.

:120

Kisha tukawazamisha baadaye walio bakia.

:121

Hakika katika haya ipo Ishara, lakini si wengi wao walio kuwa Waumini.

:122

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:123

Kina A'd waliwakanusha Mitume.

:124

Alipo waambia ndugu yao, Hud: Je! Hamchimngu?

:125

Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu.

:126

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

:127

Wala sikutakeni juu yake ujira, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:128

Je! Mnajenga juu ya kila mnyanyuko kumbusho la kufanyia upuuzi?

:129

Na mnajenga majengo ya fakhari kama kwamba mtaishi milele!

:130

Na mnapo tumia nguvu mnatumia nguvu kwa ujabari.

:131

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini.

:132

Na mcheni aliye kupeni haya mnayo yajua.

:133

Amekupeni wanyama wa kufuga na wana.

:134

Na mabustani na chemchem.

:135

Hakika mimi ninakukhofieni adhabu ya Siku Kubwa.

:136

Wakasema: Ni mamoja kwetu, ukitupa mawaidha au hukuwa miongoni mwa watoao mawaidha.

:137

Haya si chochote ila ni mtindo wa watu wa tokea zamani.

:138

Wala sisi hatutaadhibiwa.

:139

Wakamkanusha; nasi tukawaangamiza. Hakika bila ya shaka katika haya ipo Ishara. Lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

:140

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:141

Kina Thamud waliwakanusha Mitume.

:142

Alipo waambia ndugu yao Saleh: Je! Hamumchimngu?

:143

Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu.

:144

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini.

:145

Wala sikutakini ujira juu yake. Ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:146

Je! Mtaachwa salama usalimina katika haya yaliyopo hapa?

:147

Katika mabustani, na chemchem?

:148

Na konde na mitende yenye makole yaliyo wiva.

:149

Na mnachonga milimani majumba kwa ustadi.

:150

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

:151

Wala msit'ii amri za walio pindukia mipaka,

:152

Ambao wanafanya ufisadi katika nchi, wala hawatengenezi.

:153

Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa walio rogwa.

:154

Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi. Basi lete Ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

:155

Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa, na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalumu.

:156

Wala msimguse kwa uwovu, isije ikakushikeni adhabu ya Siku Kubwa.

:157

Lakini wakamuuwa, na wakawa wenye kujuta.

:158

Basi ikawapata adhabu. Hakika katika hayo ipo Ishara. Lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

:159

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:160

Watu wa Lut'i waliwakanusha Mitume.

:161

Alipo waambia ndugu yao, Lut'i: Je! Hamumchimngu?

:162

Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu kwenu.

:163

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na nit'iini mimi.

:164

Wala mimi sikutakini ujira juu yake; ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:165

Je! Katika viumbe vyote mnawaingilia wanaume?

:166

Na mnaacha alicho kuumbieni Mola wenu Mlezi katika wake zenu? Ama kweli nyinyi ni watu mnao ruka mipaka!

:167

Wakasema: Ewe Lut'i! Usipo acha, hapana shaka utakuwa miongoni mwa wanao tolewa mji!

:168

Akasema: Hakika mimi ni katika wanao kichukia hichi kitendo chenu.

:169

Mola wangu Mlezi! Niokoe mimi na ahali zangu na haya wayatendayo.

:170

Basi tukamwokoa yeye na ahali zake wote,

:171

Isipo kuwa kikongwe katika walio kaa nyuma.

:172

Kisha tukawaangamiza wale wengine.

:173

Na tukawanyeshea mvua, basi ni ovu mno mvua ya waliyo onywa.

:174

Hakika katika hayo ipo Ishara. Na hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

:175

Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

:176

Watu wa Machakani waliwakanusha Mitume.

:177

Shuaibu alipo waambia: Je! Hamfanyi mkamchamngu?

:178

Hakika mimi kwenu ni Mtume muaminifu.

:179

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, na nit'iini mimi.

:180

Wala sikutakini ujira juu yake. Ujira wangu hauko ila kwa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:181

Timizeni kipimo sawa sawa, wala msiwe katika wanao punja.

:182

Na pimeni kwa haki iliyo nyooka;

:183

Wala msiwapunje watu vitu vyao, wala msifanye jeuri kwa ufisadi.

:184

Na mcheni aliye kuumbeni nyinyi na vizazi vilivyo tangulia.

:185

Wakasema: Hakika wewe ni katika walio rogwa.

:186

Na wewe si chochote ila ni mtu tu kama sisi, na kwa yakini tunakuona wewe ni katika waongo.

:187

Hebu tuangushie vipande kutoka mbinguni ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.

:188

Akasema: Mola wangu Mlezi anajua zaidi mnayo yatenda.

:189

Basi walimkanusha, na ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.

:190

Hakika katika hayo ipo Ishara, lakini hawakuwa wengi wao wenye kuamini.

:191

Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ndiye Yeye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:192

Na bila ya shaka hii ni Uteremsho wa Mola Mlezi wa walimwengu wote.

:193

Ameuteremsha Roho muaminifu,

:194

Juu ya moyo wako, ili uwe katika Waonyaji,

:195

Kwa ulimi wa Kiarabu ulio wazi.

:196

Na hakika bila ya shaka haya yamo katika Vitabu vya kale.

:197

Je! Haikuwa kwao ni Ishara kwamba wanayajua haya wanazuoni wa Wana wa Israili?

:198

Na lau kuwa tungeli iteremsha juu ya mmoja wa wasio kuwa Waarabu,

:199

Na akawasomea, wasingeli kuwa wenye kuamini.

:200

Namna hivi tunaingiza katika nyoyo za wakosefu.

:201

Hawataiamini mpaka waione adhabu chungu.

:202

Basi itawafikia kwa ghafla, na hali hawana khabari.

:203

Na watasema: Je, tutapewa muhula?

:204

Basi, je, wanaihimiza adhabu yetu?

:205

Waonaje kama tukiwastarehesha kwa miaka,

:206

Kisha yakawafikia waliyo kuwa wakiahidiwa,

:207

Yatawafaa nini yale waliyo stareheshewa?

:208

Wala hatukuangamiza mji wo wote ila ulikuwa na waonyaji -

:209

Kuwa ni ukumbusho. Wala Sisi hatukuwa wenye kudhulumu.

:210

Wala Mashet'ani hawakuteremka nayo,

:211

Wala haitakiwi kwao, na wala hawawezi.

:212

Hakika hao wametengwa na kusikia.

:213

Basi usimwombe mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu ukawa miongoni mwa watakao adhibiwa.

:214

Na uwaonye jamaa zako walio karibu nawe.

:215

Na watwae kwa upole wanao kufuata miongoni mwa Waumini.

:216

Na ikiwa watakuasi basi sema: Mimi najitenga mbali na hayo mnayo yatenda.

:217

Na umtegemee Mtukufu Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.

:218

Ambaye anakuona unapo simama,

:219

Na mageuko yako kati ya wanao sujudu.

:220

Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia Mwenye kujua.

:221

Je! Nikwambieni nani wanawashukia Mashet'ani?

:222

Wanamshukia kila mzushi mkubwa mwingi wa dhambi.

:223

Wanawapelekea yale wanayo yasikia; na wengi wao ni waongo.

:224

Na watungaji mashairi ni wapotofu ndio wanawafuata.

:225

Je! Huwaoni kwamba wao wanatangatanga katika kila bonde?

:226

Na kwamba wao husema wasiyo yatenda?

:227

Isipo kuwa wale walio amini, na wakatenda mema, na wakamkumbuka Mwenyezi Mungu kwa wingi, na wakajitetea wanapo dhulumiwa. Na wanao dhulumu watakuja jua mgeuko gani watakao geuka.