Maktaba yote ya Kiislamu

15 - The Rocky Tract - Al-Ĥijr

:1

Alif Lam Ra. (A. L. R). Hizi ni Aya za Kitabu na Qur'ani inayo bainisha.

:2

HUENDA ikawa walio kufuru wakatamani wange kuwa Waislamu.

:3

Waache wale, na wastarehe, na iwazuge tamaa. Watakuja jua.

:4

Na hatukuuangamiza mji wowote ule ila ulikuwa na muda wake maalumu.

:5

Hawawezi watu wowote kuitangulia ajali yao, wala kuchelewa.

:6

Na walisema: Ewe uliyeteremshiwa Ukumbusho! Hakika wewe ni mwendawazimu.

:7

Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli?

:8

Sisi hatuwateremshi Malaika ila kwa sababu ya haki, na hapo hawatapewa muhula.

:9

Hakika Sisi ndio tulio teremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio tutao ulinda.

:10

Na hakika tulikwisha watumia Mitume mataifa ya mwanzo.

:11

Na hakuwafikia Mtume ila walimkejeli.

:12

Na kama hivi ndivyo tunavyo ingiza katika nyoyo za wakosefu.

:13

Hawayaamini haya, na hali ya kuwa umekwisha wapitia mfano wa watu wa kale.

:14

Na lau tungeli wafungulia mlango wa mbingu, wakawa wanapanda,

:15

Basi wangeli sema: Macho yetu yamelevywa, bali sisi wenyewe tumerogwa.

:16

Na hakika tumeweka katika mbingu vituo vya sayari, na tumezipamba kwa wenye kuangalia.

:17

Na tumezilinda na kila shetani afukuzwaye.

:18

Isipo kuwa mwenye kusikiliza kwa kuibia, naye hufuatwa na kijinga cha moto kinacho onekana.

:19

Na ardhi tumeitandaza na humo tumeweka milima, na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake.

:20

Na tumekujaalieni humo vitu vya maisha yenu, na ya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku.

:21

Na hakuna chochote ila asili yake inatokana na Sisi; wala hatukiteremshi ila kwa kipimo maalumu.

:22

Na tunazipeleka pepo za kupandishia, na tunateremsha kutoka mbinguni maji, kisha tukakunywesheni maji hayo. Wala si nyinyi mnayo yaweka.

:23

Na Sisi ndio tunao huisha na tunao fisha. Na Sisi ndio Warithi.

:24

Na tunawajua walio tangulia katika nyinyi, na tunawajua walio taakhari.

:25

Na hakika Mola wako Mlezi ndiye atakaye wakusanya. Hakika Yeye ni Mwenye hikima na Mjuzi.

:26

Na tulimuumba mtu kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yaliyo tiwa sura.

:27

Na majini tuliwaumba kabla kwa moto wa upepo umoto.

:28

Na Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika: Hakika Mimi nitamuumba mtu kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yaliyo tiwa sura.

:29

Basi nitakapo mkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia.

:30

Basi Malaika wote pamoja walimsujudia,

:31

Isipo kuwa Iblisi. Yeye alikataa kuwa pamoja na walio sujudu.

:32

(Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Iblisi! Una nini hata hukuwa pamoja na walio sujudu?

:33

Akasema: Haiwi mimi nimsujudie mtu uliye muumba kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yenye sura.

:34

(Mwenyezi Mungu) akasema: Basi toka humo, kwani hakika wewe ni maluuni!

:35

Na hakika juu yako ipo laana mpaka Siku ya Malipo.

:36

Akasema (Iblisi): Mola wangu Mlezi! Nipe muhula mpaka siku watapo fufuliwa.

:37

(Mwenyezi Mungu) akasema: Hakika wewe ni katika walio pewa muhula

:38

Mpaka siku ya wakati maalumu.

:39

Akasema: Mola wangu Mlezi! Ilivyo kuwa umenitia makosani, basi nahakikisha nitawazaini hapa duniani na nitawapoteza wote,

:40

Ila waja wako walio safika.

:41

Akasema: Hii Njia ya kujia kwangu Iliyo Nyooka.

:42

Hakika waja wangu, wewe hutakuwa na mamlaka juu yao, isipo kuwa wale wapotofu walio kufuata.

:43

Na bila shaka Jahannamu ndipo pahali pao walipo ahidiwa wote.

:44

Ina milango saba; na kwa kila mlango iko sehemu walio tengewa.

:45

Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na chemchem.

:46

(Wataambiwa:) Ingieni kwa salama na amani.

:47

Na tutaondoa chuki iliyo kuwamo vifuani mwao, wawe ndugu juu ya viti vya enzi wameelekeana.

:48

Humo hayatawagusa machofu, wala hawatatolewa humo.

:49

Waambie waja wangu ya kwamba Mimi ndiye Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.

:50

Na kwamba adhabu yangu ndio adhabu iliyo chungu!

:51

Na uwape khabari za wageni wa Ibrahim.

:52

Walipo ingia kwake na wakasema: Salama! Yeye akasema: Hakika sisi tunakuogopeni.

:53

Wakasema: Usiogope. Sisi tunakubashiria kijana mwenye ujuzi.

:54

Akasema: Mnanibashiria nami uzee umenishika! Basi kwa njia gani mnanibashiria?

:55

Wakasema: Tunakubashiria kwa haki; basi usiwe miongoni mwa wanao kata tamaa.

:56

Akasema: Na nani anaye kata tamaa na rehema ya Mola wake Mlezi ila wale walio potea?

:57

Akasema: Hebu nini amri yenu, enyi wajumbe?

:58

Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa kaumu ya wakosefu!

:59

Isipo kuwa walio mfuata Luut'i. Bila ya shaka sisi tutawaokoa hao wote.

:60

Ila mkewe. Tunakadiria huyo atakuwa miongoni watao bakia nyuma.

:61

Basi wale wajumbe walipo fika kwa Luut'i,

:62

Alisema (Luut'i): Hakika nyinyi ni watu msio juulikana.

:63

Wakasema: Bali sisi tumekuletea yale waliyo kuwa wakiyafanyia shaka.

:64

Na tumefika kwako kwa Haki, na hakika sisi tunasema kweli.

:65

Basi ondoka na ahli zako usiku ungalipo, nawe ufuate nyuma yao, wala yeyote kati yenu asigeuke nyuma. Na mwende mnapo amrishwa.

:66

Na tukamfunulia hukumu hiyo, ya kwamba hata wa mwisho wao hao ikifika asubuhi atakuwa kesha katiliwa mbali.

:67

Na wakaja watu wa mji ule nao furahani.

:68

Akasema: Hakika hawa wageni wangu, basi msinifedheheshe.

:69

Na mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi.

:70

Wakasema: Sisi hatukukukataza usimkaribishe yeyote?

:71

Akasema: Hawa binti zangu, ikiwa nyinyi ni watendaji.

:72

Naapa kwa umri wako! Hakika hao walikuwa katika ulevi wao, wakihangaika ovyo.

:73

Ukelele ukawatwaa wakipambaukiwa.

:74

Na tukaigeuza nchi juu chini, na tukawanyeshea mvua ya mawe ya udongo wa Motoni.

:75

Hakika katika hayo zipo ishara kwa waaguzi.

:76

Na miji hii ipo kwenye njia inayo pitiwa.

:77

Hakika katika hayo ipo ishara kwa Waumini.

:78

Na hakika watu wa Kichakani walikuwa wenye kudhulumu.

:79

Kwa hivyo tukawaadhibu. Na nchi mbili hizi ziko kwenye njia ilio wazi.

:80

Na bila ya shaka wakaazi wa Hijr waliwakanusha Mitume.

:81

Na tuliwapa ishara zetu, nao wakazipuuza.

:82

Nao walikuwa wakichonga majumba katika milima kwa amani.

:83

Basi ukelele ukawatwaa asubuhi.

:84

Hayakuwafaa waliyo kuwa wakiyachuma.

:85

Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake ila kwa ajili ya Haki. Na hakika Kiyama kitafika. Basi samehe msamaha mzuri.

:86

Hakika Mola wako Mlezi ndiye Muumbaji Mjuzi.

:87

Na tumekupa Aya saba zinazo somwa mara kwa mara, na Qur'ani Tukufu.

:88

Usivitumbulie macho yako vitu tulivyo waneemesha makundi fulani kati yao, wala usiwahuzunikie. Na wainamishie bawa lako (la huruma) Waumini.

:89

Na sema: Hakika mimi ni mwonyaji mwenye kubainisha.

:90

Kama hivyo tuliwateremshia walio gawa,

:91

Ambao wakaifanya Qur'ani vipande vipande.

:92

Basi Naapa kwa Mola wako Mlezi! Tutawahoji wote,

:93

Kwa waliyo kuwa wakiyatenda.

:94

Basi wewe yatangaze uliyo amrishwa, na jitenge na washirikina.

:95

Hakika Sisi tunatosha kukukinga na wanao kejeli.

:96

Hao wanao fanya kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu yupo mungu mwingine. Basi, watakuja jua!

:97

Na Sisi tunajua kwa hakika kuwa wewe kifua chako kinaona dhiki kwa hayo wayasemayo.

:98

Basi mtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi, na uwe miongoni wanao msujudia.

:99

Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie Yakini.